Thursday 30 August 2012

NADHARIA YA UPOKEZI/MWITIKIO WA MSOMAJI


NADHARIA YA UPOKEZI/MWITIKIO WA MSOMAJI
Malengo ya kazi hii ni:
(a)        Kueleza maana ya nadharia ya upokezi.
(b)        Kueleza historia fupi ya nadharia hii pamoja na kuwataja waasisi wa nadharia hii. 
(c)        Kueleza mihimili ya nadharia hii.

I.          UTANGULIZI
Nadharia inayoshughulikia upokeaji wa matini za fasihi inahusiana na ulimbwende na mitazamo ya kisaikolojia.  Kimapokeo, msomaji huwa na mawazo kuhusu matini anayopitia.  Kutokana na tajriba ya usomaji, msomaji hupata hisi maalum.  Uteuzi na upokeaji wa sanaa hushirikishwa sana na hisi kwa mujibu imani na nadharia za kilimbwende.

Ulimbwende ni mwelekeo wa kusimulia ambapo wahusika walikuwa mashujaa na wenye nguvu za ajabu na ambao walikuwa wanajeshi.


 HISTORIA FUPI YA NADHARIA YA UPOKEZI NA WAASISI WA NADHARIA             YENYEWE
Nadharia hii inayomweka msomaji katikati ya uhakiki wa fasihi ilianza miaka ya sitini na sabini ya karne ya ishirini hasa kule Marekani na Ujerumani.

Waasisi na watetezi wakuu wa nadharia hii ni Stanley Fish (1980), James Tompkins (1980), Wolfgang Iser (1974, 78) Haus Robert Jauss, Roland Barthes na wengine.  Kwa mujibu wa wavuti wa Wikipedia, wananadharia wa upokezi wanaweza kubainishwa katika makundi matatu:
(a)        Wale wanoangazia kwenye tajriba za kipekee za msomaji (Individualists).  Hawa ni           pamoja na C. S. Lewis (1961), Stanley Fish (1967) na Norman Holland (1968) ambao          walikuwa Wamarekani. 
(b)        Wale wanaofanya majaribio ya kisaikolojia kwa kikundi maalum cha wasomaji       (experimenters).  Hawa ni Reuven Tsur, Richard Gerrig, David Miall na Donald Kuiken. 
(c)        Wale wanaochukulia kwamba wasomaji wote wataipokea kazi ya fasihi kwa njia sawa.      (Uniformists).  Hawa ni Wajerumani kama vile Wolfgang Iser na Haus Robert Jauss.

Hata hivyo, Stanley Fish anadai kwamba sanaa ya maneno haichanganuliwi kwa kutumia mikakati ya jaribio la  kisayansi katika maabara. Anasema kwamba jaribio la kisayansi huonyesha ujuzi uliofanikiwa au ujuzi ambao haujafanikiwa.  Anayefanya jaribio la kisayansi huweka mpaka wa kihisia na kimawazo kati ya nafsi yake na jambo linalomshughulisha.  

       MIHIMILI YA NADHARIA YA UPOKEZI
Waitifaki wa nadharia hii huuliza maswali ambayo kwayo misingi ya nadharia hii imejengeka.  Maswali haya ni:-
(a)        Kuna uwiano wowote kati  ya maana inayosomwa na jinsi msomaji anavyoihakiki?
(b)        Je, kila kazi ya fasihi ina maana kufuatana na msomaji binafsi na jinsi anavyoichukulia?
(c)        Kuna wasomaji ambao husoma na kufasiri kazi za fasihi vizuri zaidi kuliko wasomaji wengine. 
(d)       Msomaji hutumia vigezo gani kujijulisha iwapo mawazo yake juu ya kazi fulani yanafaa au hayafai?
            Adena Rosmarin katika (Murfin 1991) anadai kuwa kazi ya fasihi ni kama kinyago ambacho hakijakamilika na kwa hivyo mchongaji hujaribu kukikamilisha. Kwa hivyo,  mhimili wa kwanza wa nadharia hii ni kwamba:
(1)        Msomaji huikamilisha kazi ya sanaa kwa kuijaliza kwa usomaji makini au kuidhalilisha       kwa usomaji wa kiholela.
            Iser na Fish wanadai kwamba kazi ya fasihi huwa na mapengo mengi ambayo msomaji      hulazimika kuyajaliza.  Kwa hivyo, msomaji hushurutika kutunga matini mpya ambazo zimechochewa kuzalika kutokana  na matini asili zilizoko kwenye kurasa. 
(2)        Nadharia hii inasisitiza athari za kazi za fasihi juu ya akili na maarifa ya mwandishi.          
 Wasomaji mbalimbali hufasiri athari hizi kupitia njia tofauti tofauti kutengemea:
            (i)         Tofauti kati ya matini na hisia za kibinafsi za msomaji. 
            (ii)        Namna matini inavyoelekezea au kutatiza mwitikio wa msomaji.  Sifa inayozua                              usomaji mzuri au mbaya wa kazi inayohusika. 
(3)        Wanadhania hawa wanashikilia kuwa kuna njia mbili za kusoma kazi ya fasihi ambazo       ni:
            (i)         Njia inayofafanua na kusisitiza mawazo ambayo kitambo yamejulikana na                          kutambuliwa na msomaji.
            (ii)        Kuwasilisha kazi ya fasihi kimafumbo ili kumchochea msomaji kujitafutia na                                  kujiamulia ujumbe uliomo katika kazi anayoisoma.  Kwa hivyo mafumbo hayo                               yanapaswa kusomwa mara kadhaa ili msomaji aelewe matini anayosoma.
(4)        Usomaji ni tendo linalofanyika na kutekelezwa kwa wakati maalum, kwamba wakati wa   kusomwa kwa matini huathiri maana ya matini hiyo.  Fish anadai kwamba wasomaji wanapasa kufanya mikataba ya aina fulani na matini hizi katika miktadha mbalimbali.     
(5)        Msomaji anayetumia mkakati wa mwitikio kusoma kazi ya sanaa hufuata hatua tatu           katika weledi wa kazi za fasihi. 
            (i)         Hurejelea kazi inayosomwa kwa tafsiri ili ithibitishwe kwamba kazi hiyo                                         inaafikiana na  yale yanayokumbukwa na msomaji. 
            (ii)        Hubainisha jinsi miktadha ya matini isiyohusiana moja kwa moja na maandishi                               inavyoweza kuhusishwa na kutangamanishwa na msomaji. 
            (iii)       Hudhihirisha kuwa maoni ya msomaji yanafungamana na mada muhimu za                                     hadithi. 
(6)        Madharia hii inazingatia usomaji, msomaji na upokezi.  Huck (1976) anadai kuwa lengo     kuu hapa ni kuwabainisha wasomaji, kuwachunguza pamoja na tendo zima la usomaji.  Kwake mvuto wa watoto kwa sanaa ni kigezo muhimu katika kutathmini ubora wa kitabu cha watoto. Naye Louis Rosenblatt (1938) katika kitabu chake Literature and Exploration anasema kuwa ni muhimu kwa mwalimu kuepuka kulazimisha kasumba au  misimamo fulani ya jinsi wanafunzi wanapaswa kuipokea kazi fulani ya fasihi. 

HITIMISHO
Baadhi ya wahakiki wa kisasa wanadai kwamba uhakiki kwa mujibu wa nadharia ya upokezi umekosa kutambua kuwa matini ina uwezo wa kupanua kuelewa kwa msomaji.  Aidha, wanadai kwamba nadharia hii imewaruhusu wasomaji kufasiri matini/kazi ya fasihi jinsi wapendavyo.  Maoni yetu hapa yanaafiki yale ya Iser (1976) aliposisitiza kuwa msomaji hana budi kuzielewa mbinu, kaida na kanuni zinazotumiwa katika kazi fulani ya fasihi ili kuweza kuisoma kikamilifu.  Kwa hivyo, nadharia hii ingali muhimu katika uhakiki wa kazi za fasihi kwa jumla. 







MAREJELEO
Bennet, Andrew (1995).  Readers and Reading.  London & New York.  Longman.
                                                   

Daiches, David (1981) Critical Approaches to Literature. London: Longman.
                                                 

Kimani Njogu et. al (1999) Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu.  Nairobi:
            Jomo Kenyatta.
                                                        

Tompkins, Jane (1980). Reader – Response Criticism. Baltimore and London: John Hopkins


Wafula, R. M & Kamau Njogu (2007).  Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi:
            Jomo Kenyatta Foundation.


Wamitila, K. W (2003) Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Books.
                                     
                       



                                                                                                               

No comments:

Post a Comment